Sunday 30 January 2011

MTINDO WA KISASA WA NYWELE UNAHARIBU AFYA ZA WANAWAKE WEUSI

Watu wa kabila la Chwi kule Ghana wanaozungumza lugha iitwayo Tshi wana methali kuhusu umuhimu wa kupendeza. Inashauri: “Ikiwa mwenda wazimu ataiba nguo zako na kukimbia nazo wakati wewe uko majini unaoga, itakuwa vyema utafute angalau kipande cha kitambaa ujifunge wakati unamkimbiza maana usipofanya vile watazamaji watadhani na wewe umeheuka.”
Hakuna mwanaume ambaye hajawahi kupayukiwa kuwa asuburi wakati ndugu yake wa kike anajipodoa akijiremba. Na kati ya mapambo yote nywele zinaongoza foleni. Mwanaume waweza kutoka bila kuchana nywele, unaweza ukawa nusu kipara (kama mimi mwandishi) lakini hujali mradi u msafi utatoka zako mitaani. Kwa mwanamke kujisanifu nywele ni tendo muhimu sana. Ndiyo maana waandishi mbalimbali wa hadithi hawakosi maelezo ya ususi ndani ya riwaya zao.

Elvis Musiba aliyefariki miezi mitatu iliyopita kaiweka taswira ya mwanamke aliyeshikilia panga na rungu juu ya jalada la “Uchu” iliyochapwa 2000. Ingawa kisa cha “Uchu” kinahusu mauaji yaliyotokea Rwanda mwaka 1994 bibiye jaladani kasuka mabutu; hakuna damu wala machozi usoni mwake. Pamoja na maudhui ya kuua kitabuni, msuko umempendeza.
Said Mohammed naye kawapamba wanawake vyema katika riwaya ya “Utengano” iliyosukwa mwaka 1980. Maimuna mtoto wa mwanasiasa fisadi anaamua kuyakimbia maisha magumu ya wazee wake na kufanya ukahaba. Ingawa anaishi vichochoroni kwenye hali ya uchafu na mavi bado chumba chake kimesanifiwa kwa picha maridadi, meza zilizosheheni vyupa vya mafuta na manukato. Kifupi ingawa anasota, mandhari ya chumba “ni powa.” Kuna wakati Maimuna kakaa akitafakari sura yake. Mwandishi anatueleza ukurasa wa 114.
“ Akajitazama kiooni. Ama kweli urembo wa kimwetu umekamilia. Hajui kwanini wanawake wengine hupiga mbio kujibabua na kujifanya mashkuli.”
Na hii ndiyo mada yetu leo. Mamilioni ya wanawake wetu weusi duniani “wanajifanya mashkuli” wakikereketwa na uzuri wa bandia kupitia tatizo la nywele. Desturi iliyoenea ni ile ya kuchoma nywele (relaxing) iliyopenyeza Bongo miaka kama hamsini iliyopita kutokea Marekani.
Z. Burhani mtunzi wa “ Mwisho wa Kosa” (1987) anasisitiza ugeni huu unavyoathiri wananchi kupitia Monika, binti aliyesoma Majuu.
“ Vijana wadogo pale mtaani nao walifurahishwa na mazungumzo na mitindo ya Monika, hata siku zote walijaribu kwenda kuzungumza na kusikiliza hadithi zake juu ya maisha ya huko Ulaya na kujaribu kuiga mitindo yake ya nguo na ya nywele.” (Ukurasa 5)
Nywele msomaji!
Nywele na mwanamke ni sawa na kucha na kidole; mti na tawi, gari na gurudumu; mchana na jua; chai na kikombe...
Kiasilia wanawake wa Kiafrika hawakuwa na tabia ya nywele bandia ndefu na laini za maiti wa India na China. Ubaya ulianzia biashara ya utumwa karne ya kumi na tano. Wanahistoria weusi wa Kimarekani wanasema Waafrika waliochukuliwa walibakia na mitindo yao ya ususi na nywele hizi zetu ngumu hadi utumwa ulipofutwa kisheria katikati ya karne ya 19. Baada ya kupewa uhuru sasa watumwa walikuwa raia wa Marekani. Tatizo likaanzaje?
Wamarekani weusi ni asilia mia 13 tu ya jamii ya nchi hiyo. Wengi jamii hiyo ni Wazungu wenye nywele ndefu laini. Sasa wanawake weusi walioshalazimika kuwa sehemu mahsusi ya raia wa taifa jipya la Marekani (lililojikomboa toka kwa Waingereza mwaka 1776) walijiona wana sura mbaya wakijilinganisha na Wazungu. Licha ya kutaka kuwa weupe, walilainisha nywele zao kutumia magadi na viazi jambo lililoleta michibuko na madhara mengi. Moja ya kanuni za wanaonyanyaswa ni kujaribu kuiga tabia za wanaowanyanyasa kusudi wasionekane kinyume cha mambo. Leo desturi hiyo ya kulainisha nywele kama za Wazungu imeenea ulimwenguni hata Tanzania.
Mwanariwaya maarufu Shafi Adam Shafi anaonyesha jamii ya Kizanzibari miaka hamsini iliyopita. Wanawake bado walithamini ususi na uzuri asilia.
Mfano mzuri ni mashoga wawili Mswahili, Mwajuma na Mhindi, Yasmin katika “Vuta Nikuvute” kitabu kilichoshinda tuzo la uandishi bora wa Kiswahili mwaka 1998:
“Yasmin alichana nywele zake vizuri akazizongazonga na kuzifungua juu zikawa kama sega la nyuki. Na Mwajuma naye alizipasua zake njia ya kati, akazifunga kwa pini huku na huku na kila mmoja kati yao alipachika kishada cha asumini kichwani.”
Tabia iliyoenea ulimwenguni leo ya wanawake weusi kulainisha nywele kutumia dawa mbalimbali zinazozilainisha, nywele bandia za maiti, kuzichoma kusudi ziangukie mabegani kama za Wazungu na Wahindi imeenezwa na wanawake weusi maarufu.
Mwaka juzi mchekeshaji wa Kimarekani, Chris Rock alitengeneza sinema maalum (“Good Hair”) kukejeli namna wanawake mashuhuri na wasanii wanavyoeneza kasumba hii kwa wanawake duniani. Chris Rock aliamua kutoa sinema baada ya binti yake wa miaka mitano kumuuliza kwanini hana nywele nzuri kama za Kizungu? Sinema hii pia inaonyeshwa kifupi katika mtandao wa You Tube, kwa watakaopenda kutazama.
Chris Rock anawahoji wanawake maarufu mathalan Oprah Winfrey mwenye nywele hizi vile vile.
Biashara ya kulainisha nywele inayapatia makampuni ya uzuri duniani fedha nyingi sana. Nchini Marekani biashara hii inaingiza dola bilioni tisa kila mwaka. Pamoja na nywele zinazouzwa toka maiti wa Kihindi na Kichina ni pia matumizi ya dawa kama “Jehri Curl” zinazosababisha michubuko ya ngozi, fuvu la kichwa na kunyofoa kabisa nywele. Kati ya magonjwa yanayotokana na usokotaji mbaya wa nywele ni “Alecopia” unaowaletea wanawake vipara miaka 35 kuendelea. Zamani wanawake wa Kiafrika walipokuwa wakisuka nywele ama kuzichana mtindo wa Afro hawakuwa na maradhi haya. Mbali na maradhi fani hii ni aghali sana. Wanawake wasiojiweza leo Bongo wanalazimika kuwa na nywele fupi na baadhi kujiona kama wana sura mbaya; kumbe sivyo. Wao ndiyo wazuri wa kweli!
Wanawake wachache maarufu mfano hayati Miriam Makeba na Angela Davis wameishi hadi uzeeni na nywele zao bila tatizo kwa kuwa hawakutumia dawa au nywele za maiti. Leo tunao baadhi ya wanawake viongozi kama kaimu balozi Umoja wa Mataifa, Asha Rose Migiro, ambaye hupigwa picha na nywele safi asilia. Baadhi ya wanawake maarufu wameanza kampeni kupinga tabia hii inayoharibu uzuri asilia mathalan Rihanna na Solange Knowels dada yake mwimbaji Beyonce aliyeamua kukata nywele na kuanza kusuka mwaka 2009. Ajabu mara Solange alipokata nywele alipingwa vikali na washabiki walioshalewa kasumba ya nywele hizi muflis.

-London, Jumapili, 23 Januari, 2011
Imetoka gazetini Mwananchi:
http://www.mwananchi.co.tz/mwananchi-jumapili/38-johari/8854-nywele-za-kisasa-zinaharibu-afya-ya-wanawake-weusi

No comments:

Post a Comment