Thursday 4 December 2014

WATANZANIA TUJIFUNZE KUWEKA AFYA MIKONONI, TUSISUBIRI KUDRA YA WAKUBWA AU MUNGU





 Miaka yote niliyosafiri na kuishi ughaibuni nimebaini siri moja  kuhusu afya. Wananchi wengi duniani hawaijali miili hadi wanapougua.  Zamani kidogo nilikuwa nikiongea na mganga wangu wa Kichina. Nilikwenda kuchomwa zile sindano zao zinazobandikwa sehemu mbalimbali mwilini na kuachwa zimesimama juu ya ngozi mithili ya mishale ya nungu nungu. Accupuncture (tamka “Akapan-kcha”), ndiyo jina lake la kitaalamu. Tiba hii iligunduliwa, kutafitiwa na kuendelezwa maelfu ya miaka kabla ya kuzaliwa Bwana Yesu Kristo na Mtume Muhammad SAW.   Kazi ya sindano hizi  ni kurekebisha na kusawazisha nguvu (au umeme) mwilini. Unapochomwa tatizo si maumivu. Haziumi kama sindano za Kizungu tulizozoea. Kinachochachafya ni vile Mchina anavyotafuta “njia sahihi.” Je, umewahi kushika waya wenye umeme? Unaukumbuka ule mstuko? Ukiwa mdogo, ndivyo  Accupuncture ilivyo. 
 Sindano za Kichina. Picha ya Mtandaoni
 

Mbali na sindano mganga  huacha taa  zikichoma juu ya zile sindano. Ingawa husikii maumivu yeyote, kinachofanyika huiathiri  mitiririko ya mifereji yako asilia. Ikiziba, ndipo mtu hupatwa maradhi. Muundo mzima wa tiba za Kichina (na Mashariki mathalan Ayudervic ya Wahindi) ni tofauti na tuliouzoea wa sayansi ya Kizungu. Unapoingia chumba cha daktari wa Kizungu (au aliyesomea mfumo wa Kizungu) anachotazama ni  namna ya kutatua.  Unadungwa sindano au unapewa vidonge.  Bas.
 Mambo yamekwisha. Tiba za Kichina ziko kinyume. Utaombwa utoe ulimi nje. Utachunguzwa wekundu wake,  nchani. Mkali sana au hafifu? Hapo atajua hisia zako zikoje. Atakunusa. Atakuuliza unalalaje? Ndoto zako, zikoje.  Atataka kujua  unapokula chakula kina vitu gani. Je mna binzari na pilipili?
Utaratibu  wa tiba za Kichina umeanza kupokelewa kutokana na dawa za Kizungu kudhuru au kuwa sugu kwa virusi.  Miaka kama kumi iliyopita nilikuwa na maumivu makali shingoni,  chini ya sikio. Bahati nzuri daktari wangu wa Kizungu alikuwa aina ya wale matabibu walioanza kufunguka macho. Baada ya kunipima moyo, sikio, kichwa na kadhalika akakiri hakuna noma.  Hakunipa dawa. Hakunichoma sindano.
“Nenda kwa msingaji akakukande,” akaasa. Na kweli msingaji akaniuliza vipi ninafanya kazi gani. Nikamwambia muziki. Kutokana na kazi ya kupinda bega moja ninapopiga gitaa, au kuinama kinamna ninapotwanga ngoma au piano,  vyote viliathiri shingo na mabega. Baada ya kusingwa mara  kadhaa ikawa neema, lakini mwezi mmoja kwisha, yakarejea tena. Nilipokwenda kwa Mchina alinipachika hizo sindano za Accupuncture.  Sijalisikia tena tatizo; hadi kesho.  Ingekuwa zamani, waganga wa Kizungu wangenipa tu dawa za kupunguza maumivu ambazo hazingemwondoa mjusi kafiri. 

Sisi Waafrika, hali kadhalika, tuna  tiba zetu asilia. Walakin,  tumezitupilia mbali.Matokeo tiba zetu  zimechujwa badala yake zikabakizwa imani za ushirikina tunazozitumia kulogana na kufanyiana uhayawani. Kama kuua Albino.
Wachina nao walitawaliwa na wageni. Mwanzo wa karne ya 20 kwa mfano, tiba asilia za Kichina (mseto wa miti shamba na Accupunture) zilitupwa shimoni. Wenyeji wakaenzi, sayansi za Kizungu. Wakati wa vita vya mapinduzi yaliyoongozwa na Mwenyekiti Mao Ze Dung miaka ya Thelathini maradhi na majeraha hayakuponyeka. Ndipo serikali mpya iliyoundwa 1947 ikarejesha tiba asilia.  China leo inasifika (na kuuza) tiba zake asilia sehemu mbalimbali za dunia; tena aghali.
Mwongozo mzima wa Wachina umelala katika kinga.  Hiyo hiyo, Accupuncture ambayo sisi huchomwa tunapougua wao hufanyiwa kinga maradhi. Anayeonja asali huchonga mzinga.
“Kazi yake,” alinieleza Dr Xin (aliyeshastaafu), “ni kurekebisha mtiririko wa umeme wa nguvu mwilini.Si lazima uwe mgonjwa. Hata watoto wadogo wamezoea.”
Ukiacha tiba hii ya  nungu nungu, kuna  mazoezi ya viungo na sanaa. Mfano mzuri ni wazee. Hufanya mazoezi ya viungo yanayoitwa Tai Chi Chuan; aina ya dansi taratibu inayojenga msingi na uwiano na ustahilimivu wa mifupa. Juu yake wazee hushauriwa kujifunza kuchora, kupiga chombo  cha muziki, mahesabu, nk.
 Dr Xin alisisitiza kwa vile ubongo wa mwanadamu nao huzeeka,  kujifunza kitu kipya baada ya miaka sitini au sabini huujenga. Jingine, ulaji wa miti shamba. Mfano, mimea iitwayo Gingko na Cordyceps. 
Majani ya Gingko. Picha ya Mtandaoni

Cordyceps ni aina ya Uyoga unaosaidia viini vya mishipa ya damu na kukomaza kinga maradhi kupitia ini na viungo vya tumbo. Gingko ni mti mkubwa unaoota China, Japan na Korea, takribani miaka  270 milioni sasa. Una nguvu na uwezo kiasi ambacho wadudu hushindwa kuushambulia.  Bomu la Atomiki lilipopasuliwa Japani mwaka 1945, baadhi ya viumbe ambavyo havikuharibika  ni miti ya Gingko. Ingawa iliunguzwa,  mizizi na mashina yake yalinyauka tena na mengi yangali hai, leo. Gingko hutumiwa kuimarisha ubongo na kutibu kupotelewa kumbukumbu hasa kwa wazee na watu waliovuta bangi kipindi kirefu.  Si ajabu wenzetu China na Japan huishi kitambo sana.
Fundisho nini?
Kazi ya waganga na hospitali ni kututibu. Ila sehemu kubwa ya siha yetu inatutegemea sisi wenyewe. Kijarida kinachosambazwa sehemu mbalimbali Uingereza  kinasisitiza  maradhi yanayopunguza au kuondoa kabisa maisha yetu,(mbali na UKIMWI, Malaria na aina kadhaa za Saratani) ni moyo, shinikizo la damu, kisukari na figo kutokana na kutojiangalia sawasawa.
 

 Chapati na sambusa..mfano wa vyakula vya wanga tulivyozoea. Vyahitaji kusaidiana na mboga mboga hata kama wala nyama.

Ushauri unaotolewa kuepuka madhila ni kutovuta sigara, unene, kufanya mazoezi ya viungo na kuangalia damu. Damu ikipimwa  iwe chini ya vipimo 120 au isipite 80. Vipimo hivi vinavyoitwa “sytolic” na “diastolic” huangalia mishipa ya damu inavyokwenda.  Mbali na mazoezi ya viungo ushauri unaotolewa ni kupunguza chumvi  na kunywa maji. Chumvi nyingi husababisha shinikizo la damu au saratani ya tumbo. Chumvi nyingi ni zaidi ya gramu 1.5; yaani kijiko kimoja au viwili vya chai kwa siku kwa mtu mmoja.
 
Mseto wa mboga za matango, nazi na mbegu mbichi za Mlozi. Mseto bab kubwa huu kwa Salad. Rutuba ya madini mwilini kusaidia mifupa, ngozi, nywele, nguvu za urijali, ngono, nk ...

 Jingine muhimu ni kufanya vitendo vinavyoendesha mapigo yako ya moyo  na mapafu kwenda haraka dakika 30, mara tano, kwa juma. Mazoezi ya viungo au kutembea haraka.  Unasisitiziwa ule  aina tano za matunda na mboga kwa siku kuhakikisha uzito unabakia kawaida. Wengi wetu hula zaidi vyakula vya wanga au nafaka, lakini hatuzingatii  mboga mbichi za majani na matunda. Unene huchangia shinikizo la damu. Kupunguza unene, jaribu kula nyama zisizo na mafuta, nyama za kukaanga. Unapokula vyakula vilivyokaangwa hakikisha pia unapata mboga au maharage na kunde ili kupunguza mafuta ya wanyama ambayo si mazuri mwilini.
  














               

No comments:

Post a Comment