Monday 23 November 2015

FAB MOSES - MTABIRI WA LONDON ALIYETUNGA WIMBO WA KUSHINDA MAGUFULI


Wakati kampeni za uchaguzi zikiendelea miezi kadhaa iliyopita, Mtanzania mmoja mkazi London alikuwa na mtazamo tofauti. Mwanamuziki na mcheza sarakasi huyu  anaitwa Fab Moses.
“Nyinyi semeni yenu mnayotaka, lakini CCM na Bw John Pombe Magufuli watashinda tu.”
Rais wa Jamhuri ya Tanzania,  J P Magufuli.   Picha ya Blog la Yinga Boy


Fab Moses si maarufu kwa utabiri bali kwa ucha Mungu wake, upole na ukarimu. Si wale wanaojifaragua au kupiga kelele mbele za watu. Mtaratibu anayejishughulisha na kazi mbalimbali za ajira  za uchovu tosha. Chukua mfano siku niliyomtembelea kwake kumfanyia mahojiano haya. Ilibidi miadi ipangwe saa tisa alasiri, maana aliingia kitandani asubuhi hiyo baada ya kazi ya usiku kucha.


“Ukiwaeleza Bongo kazi tunazofanya hawawezi kuamini,” Fab Moses alisema akitabasamu bila nadama, majuto au kauli mbaya, “Wanadhani Ulaya ni kula kuku tu? Nimeingia kazini  usiku wakati wenzangu wanakoroma.”

Moja ya kazi azifanyazo ni  usambazaji wa bidhaa ambapo huendesha gari inayoinulia bidhaa juu ya ardhi  iitwayo “fork lift ” kwa kimombo. Ilibidi asomee kazi hiyo ingawa tayari alikuwa dereva. Hurudi asubuhi hoi. Mtanzania huyu hufanya pia shughuli nyingine za sulubu kama kusambaza magazeti madukani. Lakini kipajhi chake mahsusi, Fab Moses ni kucheza sarakasi, utunzi wa mashairi na nyimbo za Kiswahili anazoziimba kwa sauti inayoghani. Huimba vile vile nyimbo  maarufu za  Afrika Mashariki mathalan, Sina Makosa, Kalubandika,  Rosa Nenda Shule nk. Mara kwa mara huwa na bendi maarufu ya Watanzania, Wakenya na  Wakongo, “Afrika Jambo”  aliyoiasisi na  mpiga gitaa maarufu Kawele Mutimanwa na wanamuziki wengine : bwana besi Billy Mwangura (Kenya) na RamaSax – mpiga sax m wa Tanga aliyekuwa zamani  kikosi cha Simba Wa Nyika.
Jina  la “Afrika Jambo” alilibuni yeye Fab Moses.
Fab Moses akiimba na gwiji mwingine wa muziki wa kijadi wa Tanzania, Saidi Kanda. 
Picha na Jonathan Pace.
Kabla ya Afrika Jambo, Fab Moses alikuwa pamoja na Kawele Mutimanwa ndani ya bendi ya No Tchuna Cha iliyotoa albam ya “ Alama Za Vidole” mwaka 1998.
Ukiacha bendi hizi na muziki, Fab Moses ameendesha kikundi cha wanasarakasi watatu- The High Flyers (Wapaa Juu), miaka mingi.
Leo anapofanya maonesho yeyote (mbali ya sauti yake  inayolinganishwa na  ya marehemu nguli Marijani  Rajabu) lazima Fab Moses atoke mzima mzima, atembee kwa mikono, ajirushe , huku akipigiwa makofi , ngoma na vigelegele.
Hivyo ndivyo maisha ya wanamuziki  Ulaya huwa. Siku moja moja atakuwa jukwaani akitumbuiza, nyingine akimenyeka kutafuta fedha ya kulipia nyumba, gari, bima, chakula  na familia.  Maisha ya Uzunguni mazuri – ila ghali na kila kitu huenda kwa muda, muda na muda tena.
Ndani ya haya maisha, aghalabu, yanayodai nidhamu ya saa mkononi na mbio miguuni, hutafutwa wasaa  wa kwenda studio kurekodi. Studio za muziki Majuu ni nzuri ila aghali sana. Kiwastani studio kubwa, safi, hudai paundi 150 kwa siku (kama shilingi laki nne). Ukitaka za bei rahisi, uchochoroni, labda nyumbani kwa mwanamuziki mwingine mwenye vyombo, huwa kama paundi 50 kwa siku yaani shilingi laki moja na robo. Na hizi ni za kubabaisha babaisha, maana vyombo si vya hali ya kuridhisha sana.  Pamoja na pepesa pepesa hiyo, Fab Moses  keshajitahidi kutoa albam yake ya nyimbo kede  kede za Kiswahili iitwayo “Nengua”...niliwahi kuhakiki CD hii ilipotoka 2010. Kati ya waliofagilia “Nengua” ni mfanyabiashara  wa Kiganda John Kizito, aliyechangia baadhi ya  gharama.
Bw Kizito : “Fab Moses ananikumbusha wananamuziki wa Kiswahili wa zamani. Hapigi makelele wala hachanganyi matusi na maneno ya Kiingereza. Tena kajaaliwa sauti nzuri sana.”

Ndani ya muktadha huu ndipo Fab Moses akaamua kujitolea kutunga wimbo wa kuchangia uchaguzi wa Mheshimiwa John Pombe Magufuli. Wimbo huo unaoweza kusikika katika mtandao wa You Tube, unaitwa “Magufuli CCM”
Unaanza na maneno na sauti yake inayofanana na ya marehemu Marijani Rajabu mwana Sokomoko
CCM Oyee
CCM Kanyaga
Kanyaga! Kanyaga! Kanyaga! Kanyaga!
Kidumu kidumu chama cha Mapinduzi....”
Baada ya muda  wosia kwa Mheshimiwa John Magufuli.
“Baba Magufuli ushike chombo bahari ni kubwa usituache sasa tukaangamia
Bahari ni kubwa yenye papa na nyangumi wenye uchu wa madaraka Baba...”
Hapo maneno yanachimba anapokwenda ndani ya maudhui ya chama  na sababu gani baadhi yetu Watanzania tuna imani na CCM.
“Angalia Somalia – wanachinjana
Kule Congo- Zaire- wanachinjana
Sudan Ooh- Wanachinjana!
Kwa Gaddafi Libya-wanachinjana!”
Ujumbe mkubwa wa maneno haya ni kwamba ingawa wapo tusiopenda CCM na wale tuliotaka isishinde uchaguzi mwezi uliopita, CCM imehakikisha Tanzania nchi ya amani. Ndiyo kisa cha kuyataja mataifa yenye tafrani : Somalia, Congo, Sudan , Libya nk
Wimbo huu uliochangamka sana umechangia gitaa la Mkongo ajulikanye kwa jina la Burkina Faso.
Fab Moses ana kipaji cha utunzi wa mashairi na kuimba lakini hakusoma sana. Alimaliza shule ya msingi, Tandale , Manzese. Angali bado shuleni na miaka kumi na moja, alianza kujifunza kuruka ruka na kucheza sarakasi mwaka 1980.
“Enzi hizo tulitumia pumba za mahindi kuangukia (kama kitanda) mitaani.  Baada ya muda nilipojiamini zaidi nilianza kwenda na wenzangu mitaani kufanya maonesho yaliyoitwa mwaga mwaga. “
Fab Moses akitembea kwa mikono katika moja ya maonesho yake Uingereza wakati wa tamasha la kutimiza miaka 40 ya urafiki kati ya Uingereza na Tanzania, Novemba 2015. Picha ya Jonathan Pace

Walikuwa wakiruka wanarushiwa fedha na hatimaye  mwaka 1982 Fab Moses alichukuliwa na kiwanda cha majembe cha UFI na kuanza kupata mafunzo rasmi. Hatimaye alihama hama mashirika mengine ya umma mfano Bandarini na Urafiki ambapo kulikuwa na vifaa na taaluma zaidi. Taaluma ilipokomaa mwaka 1984 sasa alicheza na vikundi  vikubwa vikubwa mathalan Super Mwongozo, Kigongo cha Mpingo, Super Fanaka  na hatimaye Makutano chini ya hayati mzee Kingalu Ghadhaba aliyewaboresha vijana zaidi.
 Ni katika kipindi hiki alipokuwa akihudhuria mazoezi  na maonesho ya bendi maarufu iliyoongozwa na Marijani Shaban, Dar International.  Humo humo pia alianza kuimba nyimbo za Taarabu na kikundi cha Bima taarabu kwa mfano. Baada ya kutembelea sehemu kadhaa nchini ikiwemo ziara ya muda mrefu Mwanza mwaka 1988 ndipo ikaja safari ya kwendas Ujerumani na kikundi cha sarakasi cha Black Scorpions. Maonesho ya nchi mbalimbali barani Ulaya hatimaye yalimshusha Uingereza anapokanyaga hadi leo. 
SIKILIZA WIMBO HUSIKA  HAPA




No comments:

Post a Comment